Jeremiah 50:7-17

7 aYeyote aliyewakuta aliwala;
adui zao walisema, ‘Sisi hatuna hatia,
kwa kuwa wao walitenda dhambi dhidi ya Bwana, malisho yao halisi,
Bwana, aliye tumaini la baba zao.’

8 b“Kimbieni kutoka Babeli;
ondokeni katika nchi ya Wakaldayo
tena kuweni kama mbuzi wale waongozao kundi.
9 cKwa maana nitaamsha na kuleta dhidi ya Babeli
muungano wa mataifa makubwa kutoka nchi ya kaskazini.
Watashika nafasi zao dhidi yake,
naye kutokea kaskazini atatekwa.
Mishale yao itakuwa kama mishale ya mashujaa walio hodari,
ambao hawawezi kurudi mikono mitupu.
10Kwa hiyo Ukaldayo utatekwa nyara;
wote wamtekao nyara watapata za kutosha,”
asema Bwana.

11 d“Kwa sababu hushangilia na kufurahi,
wewe utekaye urithi wangu,
kwa sababu unachezacheza kama mtamba anayepura nafaka,
na kulia kama farasi dume,
12 emama yako ataaibika mno,
yeye aliyekuzaa atatahayari.
Atakuwa mdogo kuliko mataifa mengine yote,
atakuwa nyika, nchi kame na jangwa.
13 fKwa sababu ya hasira ya Bwana hatakaliwa na mtu,
lakini ataachwa ukiwa kabisa.
Wote watakaopita Babeli watatiwa hofu na kudhihaki
kwa sababu ya majeraha yake yote.

14“Shikeni nafasi zenu kuzunguka Babeli,
enyi nyote mvutao upinde.
Mpigeni! Msibakize mshale wowote,
kwa kuwa ametenda dhambi dhidi ya Bwana.
15 gPiga kelele dhidi yake kila upande!
Anajisalimisha, minara yake inaanguka,
kuta zake zimebomoka.
Kwa kuwa hiki ni kisasi cha Bwana,
mlipizeni kisasi;
mtendeeni kama alivyowatendea wengine.
16 hKatilieni mbali mpanzi kutoka Babeli,
pamoja na mvunaji na mundu wake akivuna.
Kwa sababu ya upanga wa mdhalimu
kila mmoja na arejee kwa watu wake mwenyewe,
kila mmoja na akimbilie
kwenye nchi yake mwenyewe.

17 i“Israeli ni kundi lililotawanyika
ambalo simba wamelifukuzia mbali.
Wa kwanza kumla alikuwa mfalme wa Ashuru,
wa mwisho kuponda mifupa yake
alikuwa Nebukadneza mfalme wa Babeli.”
Copyright information for SwhNEN